Habari | 08.07.2008 | 15:00 UTC
Viongozi wa G8 waafikiana kupunguza gesi za viwanda ifikapo 2050
Toyako/Japan
Viongozi wa nchi 8 tajiri zaidi duniani kiviwanda wanaoendelea na mkutano wao nchini Japan, wamesema wanaazimia kupunguza gesi zinazoharibu mazingira ang'alau kwa nusu ifikapo mwaka 2050. Katika taarifa yao ya pamoja, viongozi hao wamesema wanahitaji kuweka mikakati ya kufikia mtazamo wa pamoja juu ya suala hilo, ila hawakutoa shabaha zao.
Taarifa hiyo imekaribishwa na Umoja wa Ulaya ila imekosolewa na wanaharakati wa kulinda mazingira. Fuko la fedha la mazingira duniani WWF limeieleza taarifa hiyo kuwa ya kuskitisha na kwamba nchi tajiri zimekuwa zikiyumbisha juhudi zao.
Lakini kwa mujibu wa katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Ban-Ki-Moon, mbali na tatizo hilo la mabadiliko ya hali ya hewa itokanayo kwa sehemu kubwa na gesi ya kaboni, dunia sasa inakabiliwa na matatizo matatu kwa pamoja ambayo ni budi yatatuliwe kwa pamoja.






