| 16.05.2008 | 15:00 UTC
Kamishna wa umoja wa Ulaya wa misaada aenda Burma.
Rangoon.
Kamishna wa maendeleo wa umoja wa Ulaya ameutaka utawala wa kijeshi wa Burma kuruhusu wafanyakazi wa kutoa misaada kuingia nchini humo ili kusaidia wahanga wa kimbunga kilicholeta maafa makubwa.
Afisa wa umoja wa Ulaya amesema kuwa Louis Michel ametumia mkutano wake na maafisa wa kijeshi wa utawala wa Burma mjini Rangoon kuutaka utawala huo kutoa visa kwa wataalamu wa kutoa misaada wa umoja wa Ulaya pamoja na uhuru wa kusafiri kwa mashirika ya kutoa misaada ya umoja wa Ulaya.
Michel ameomba kufanya mkutano na waziri mkuu wa Burma pamoja na waziri wa mambo ya kigeni, na kuomba ruhusa ya kutembelea eneo lililoshambuliwa na kimbunga hicho la Irrawaddy, ambalo liliathirika sana na kimbunga Nargis karibu wiki mbili zilizopita.
Mashirika ya kimataifa ya kutoa misaada yamesema kuwa wahanga milioni 2.5 wa kimbunga hicho wanahitaji msaada wa haraka. Idadi rasmi ya watu waliokufa hadi sasa imefikia 43,000, lakini mashirika ya kimataifa yanasema kuwa idadi halisi inaweza kuwa zaidi ya watu 100,000.






