News | 16.05.2008 | 15:00 UTC
Bush - Israel yaweza kuitegemea Marekani.
Jerusalem.
Rais Bush wa Marekani ameliambia bunge la Israel kuwa Marekani itasimama pamoja na Israel katika kuipinga Iran iwapo itajaribu kujipatia silaha za kinuklia.
Bush ameongeza kuwa anakichukulia kwa umuhimu wa juu kitisho kilichotolewa na rais wa Iran Mahmoud Ahmedinejad kuifuta Israel kutoka katika ramani ya dunia. Akizungumza umuhimu wa kuitetea Israel katika mashariki ya kati Bush amesema.
O-Ton Bush
Iran imesema kuwa mpango wake wa kinuklia una lenga katika matumizi ya umeme.
Bush, ambaye yuko katika ziara kuadhimisha kuasisiwa kwa taifa la Israel miaka 60 iliyopita, ameliambia bunge la Israel , Knesset kuwa Israel pia inaweza kutegemea uhusiano usiolegalega na Marekani.
Rais Bush ameondoka nchini Israel alielekea nchini Saudi Arabia leo kuanza ziara nchini humo , ambayo itakuwa ni maadhimisho ya miaka 75 ya uhusiano baina ya Marekani na nchi hiyo ya Kifalme.
Bin Laden awashutumu viongozi wa mataifa ya magharibi kuhusu miaka 60 ya Israel
Dubai.
Kiongozi wa kundi la kigaidi la Al-Qaeda Osama bin Laden amewashambulia viongozi wa mataifa ya magharibi kwa kushiriki katika maadhimisho ya miaka 60 ya kuasisiwa kwa taifa hilo la Kiyahudi.
Akizungumza katika ujumbe wa katika radio leo Ijumaa , bin Laden ameapa kuendeleza mapambano dhidi ya taifa hilo la Kiyahudi pamoja na washirika wake na kwamba Waislamu hawatasalim amri hadi pale Palestina itakapokombolewa kabisa.
Ujumbe huo leo umekuja wakati rais wa Marekani George W. Bush anakamilisha ziara yake nchini Israel kuadhimisha miaka 60 tangu kuasisiwa kwa taifa hilo.
Bin Laden amesema katika ujumbe huo kuwa mapambano kwa ajili ya Palestina ni jambo linalosukuma vita vya Al-Qaeda dhidi ya mataifa ya magharibi.
Rais wa China aenda katika eneo la tetemeko.
Beijing.
Rais wa China Hu Jintao amekwenda katika mji wa Mianyang katika jimbo la Sichuan kuona binafsi maafa yaliyotokea siku ya Jumamosi baada ya tetemeko la ardhi kutokea katika eneo hilo.
Vyombo vya habari vya serikali vimeripoti kuwa rais Hu ametoa wito wa kuongezwa juhudi katika kile alichokieleza kuwa ni awamu muhimu ya operesheni ya uokozi.
Maafisa sasa wanasema , wanahofu kuwa idadi ya watu waliokufa inaweza kuwa juu zaidi ya 50,000.
Hadi sasa , kiasi cha watu 22,000 wamethibitishwa kuwa wamefariki, lakini watu wengine kwa maelfu hawajulikani waliko. Mji wa Mianyang umekuwa kituo cha kupokea watu walionusurika wanaomiminika kutoka katika maeneo yaliyoathirika karibu na eneo tetemeko hilo lilipotokea kilometa 100 upande wa magharibi.
Kamishna wa umoja wa Ulaya wa misaada aenda Burma.
Rangoon.
Kamishna wa maendeleo wa umoja wa Ulaya ameutaka utawala wa kijeshi wa Burma kuruhusu wafanyakazi wa kutoa misaada kuingia nchini humo ili kusaidia wahanga wa kimbunga kilicholeta maafa makubwa.
Afisa wa umoja wa Ulaya amesema kuwa Louis Michel ametumia mkutano wake na maafisa wa kijeshi wa utawala wa Burma mjini Rangoon kuutaka utawala huo kutoa visa kwa wataalamu wa kutoa misaada wa umoja wa Ulaya pamoja na uhuru wa kusafiri kwa mashirika ya kutoa misaada ya umoja wa Ulaya.
Michel ameomba kufanya mkutano na waziri mkuu wa Burma pamoja na waziri wa mambo ya kigeni, na kuomba ruhusa ya kutembelea eneo lililoshambuliwa na kimbunga hicho la Irrawaddy, ambalo liliathirika sana na kimbunga Nargis karibu wiki mbili zilizopita.
Mashirika ya kimataifa ya kutoa misaada yamesema kuwa wahanga milioni 2.5 wa kimbunga hicho wanahitaji msaada wa haraka. Idadi rasmi ya watu waliokufa hadi sasa imefikia 43,000, lakini mashirika ya kimataifa yanasema kuwa idadi halisi inaweza kuwa zaidi ya watu 100,000.
Mzozo wa Chavez na Merkel wagubika mkutano wa L.America.
Lima.
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ameahidi msaada kutoka Ujerumani kwa ajili ya wizara ya mazingira nchini Peru wakati wa mkutano na rais wa nchi hiyo, Alan Garcia.
Kufuatia mazungumzo ya viongozi hao wawili, Garcia ameeleza kumuunga kwake mkono Merkel katika mvutano wake wa hivi karibuni na rais wa Venezuela Hugo Chavez.
Merkel anatarajiwa kukutana na Chavez , kandoni mwa mkutano wa umoja wa Ulaya na mataifa ya Latin Amerika unaofanyika leo Ijumaa katika mji mkuu wa Peru , Lima.
Mkutano huo unatarajiwa kujadili umasikini na mabadiliko ya hali ya hewa, lakini umegubikwa na mzozo kati ya viongozi hao wa Ujerumani na Venezuela. Merkel amezitaka nchi za eneo hilo kujiweka mbali na serikali ya kisishalist ya Venezuela, wakati Chavez amemshutumu Merkel kwa kuwa katika utamaduni ule ule wa kisiasa wa enzi za Nazi.
uchaguzi wa duru ya pili Zimbabwe Juni 27
Harare.
Tume ya uchaguzi nchini Zimbabwe imesema leo kuwa uchaguzi wa rais wa duru ya pili utafanyika Juni 27.
Kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai anatarajiwa kurejea nchini Zimbabwe kesho Jumamosi baada ya kuwapo nje ya nchi hiyo kwa muda wa zaidi ya mwezi mmoja kufuatia uchaguzi unaobishaniwa.
Tsvangirai ambaye hivi sasa yuko nchini Ireland ya kaskazini, anatarajiwa kurejea nchini humo na atawasili mjini Harare mchana, kwa mujibu wa mkurugenzi wa habari wa chama cha MDC Luke Tamborinyoka.
Baada ya uchaguzi wa March 29 kumekuwa na ghasia ambapo chama cha upinzani cha MDC , kinalaumu wanajeshi wa utawala utawala wa Zimbabwe.
Chama cha upinzani kinasema wanachama wake 40 wameuwawa na zaidi ya nyumba 1,000 zimeharibiwa ama kuvunjwa.
Chama cha ZANU -PF cha rais Robert Mugabe kimekanusha kuhusika na kukilaumu chama cha MDC kwa kuanzisha ghasia katika juhudi za kulichafua jina la rais Mugabe.
Umoja wa mataifa kurejea Somalia.
New York.
Baraza la usalama la umoja wa mataifa limepitisha azimio ambalo linaweza kufungua njia kuwekwa kwa wanajeshi wa umoja wa mataifa wa kulinda amani nchini Somalia.
Licha ya kuwa maandishi ya azimio hilo hayatoa ahadi ya kuwekwa kwa jeshi la umoja wa mataifa, lakini linatoa wito kwa umoja wa mataifa kupanga kuchukua jukumu la ujumbe wa kulinda amani ambao kwa sasa unaendeshwa na umoja wa Afrika.
Pia azimio hilo linatoa wito kwa taasisi hiyo ya dunia kurejesha operesheni zake za kisiasa katika nchi hiyo iliyoharibiwa na vita kutoka nchi jirani ya Kenya. Serikali ya Somalia inayoungwa mkono na Ethiopia, imekuwa ikipambana na wapiganaji wa Kiislamu tangu mwaka 2006.
Mkutano wa mataifa ya Ulaya na latin Amerika waanza.
Lima.
Viongozi kutoka mataifa 50 ya Ulaya , Amerika ya kusini na Caribik, wanakutana mjini Lima , Peru kujadiliana kuhusu umasikini, mabadiliko ya hali ya hewa na kuongezeka kwa bei za vyakula duniani. mkutano huo huenda ukashindwa kufikia makubaliano juu ya majadiliano ya kibiashara.
Tayari kikao hicho cha leo na kesho kimefunguliwa kwa mabishano miongoni mwa viongozi wa eneo hilo kuhusiana na biashara huria.
Halikadhalika malumbano kati ya rais Hugo Chavez na kansela wa Ujerumani Angela Merkel.Mwenyeji wa mkutano huo rais Alan Garcia wa Peru, amesema viongozi pia watajadiliana juu ya hali za kibinadamu.
Ameongeza kuwa masuala yatakayozingatiwa ni pamoja na hali za binadamu katika maendeleo ya teknolojia, utajiri na demokrasia pamoja na hali bora za kiutu.Rais Garcia pia amemtetea kansela wa Ujerumani Angela Merkel katika malumbano yake na kiongozi wa Venezuela Hugo Chavez.
O-Ton Garcia.
Hata hivyo kansela wa Ujerumani amesema kuwa anataka kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na eneo hilo na pia kuwa na masikilizano na Chavez katika kikao cha leo kitakachofanyika pembezoni mwa mkutano huo.
Mivutano inayoongezeka kati ya viongozi wa eneo hilo la Amerika ya kusini inatishia kugubika makubaliano yoyote ya mwisho.
Viongozi hasimu wa Lebanon kukutana Qatar.
Beirut.
Viongozi wa makundi hasimu ya kisiasa nchini Lebanon wanatarajiwa kukutana nchini Qatar kwa mazungumzo yenye lengo la kutatua mzozo ambao umeisukuma nchi hiyo katika ukingo wa vita vipya vya wenyewe kwa wenyewe.
Mkutano huo ni sehemu ya makubaliano yaliyopatanishwa na jumuiya ya nchi za Kiarabu siku ya Alhamis, ambayo yamemaliza mapigano baina ya wapiganaji kutoka kundi la upinzani la Washia la Hezboullah na waungaji mkono serikali inayoungwa mkono na mataifa ya magharibi.
Zaidi ya watu 60 wameuwawa na wengine kadha wamejeruhiwa katika mapigano mabaya kabisa kuwahi kutokea nchini Lebanon tangu wakati wa vita vya mwaka 1975-1990.
Mapigano hayo yalizushwa na hatua za serikali kuzuwia nguvu za kundi la Hezboullah.
Serikali imefuta hatua hizo. mzozo wa kisiasa ulianza mwishoni mwa mwaka 2006 wakati mawaziri wanaounga mkono Syria walipotoka katika baraza la mawaziri.
Nchi hiyo imekuwa bila kiongozi wa serikali tangu pale muda wa rais wa zamani Emile Lahoud ulipomalizika Novemba mwaka jana. Bunge la nchi hiyo limeshindwa hadi sasa kumchagua mrithi wake.
dalai Lama atoa wito wa kujitawala zaidi Tibet
Bochum, Ujerumani.
Kiongozi wa kidini wa Tibet Dalai lama anaendelea na ziara yake ya siku tano nchini Ujerumani akiwa katika mji wa Bochum.
Kiongozi huyo wa kidini amewashukuru waungaji wake mkono katika bara la Ulaya wakati kwa mara nyingine tena amesisitiza kuwa anatafuta kujitawala zaidi kwa jimbo lake la Tibet, na sio uhuru kamili.
Jana Alhamis Dalai Lama alikutana na viongozi wa kisiasa wa eneo la Ulaya pamoja na rais wa bunge la Ujerumani, Nobert Lammert.
China tayari imepinga mipango ya kukutana siku ya Jumatatu na waziri wa maendeleo wa Ujerumani Heidemarie Wieczorek-Zeul.
Mwaka jana kansela Angela Merkel alikutana na Dalai Lama mjini Berlin, hatua ambayo ilisababisha uhusiano kati ya China na Ujerumani kuingia dosari.






